Mhubiri

1 Maneno ya Mhubiri mwana wa Daudi,mfalme katika Yerusalemu.
2 Mhubiri asema, Ubatili mtupu, ubatili mtupu, mambo yote ni ubatili.
3 Mtu ana faida gani ya kazi yake yote aifanyayo chini ya jua?
4 Kizazi huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima.
5 Jua lachomoza, na jua lashuka, na kufanya haraka kwenda mahali pa maawio yake.
6 Upepo huvuma kusi, hugeuka kuwa kaskazi; hugeuka daima katika mwendo wake, na upepo huyarudia mazunguko yake.
7 Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.
8 Mambo yote yamejaa uchovu usioneneka, jicho halishibi kuona, wala sikio halikinai kusikia.
9 Yaliyokuwako ndiyo yatakayokuwako; na yaliyotendeka ndiyo yatakayotendeka; wala jambo jipya hakuna chini ya jua.
10 Je! Kuna jambo lo lote ambalo watu husema juu yake, Tazama, ni jambo jipya? Limekwisha kuwako, tangu zamani za kale zilizokuwa kabla yetu sisi.
11 Hakuna kumbukumbu lo lote la vizazi vilivyotangulia; wala hakutakuwa na kumbukumbu lo lote la vizazi vitakavyokuja, miongoni mwao wale watakaofuata baadaye.
12 Mimi, Mhubiri, nalikuwa Mfalme wa Israeli katika Yerusalemu.
13 Nikatia moyo wangu ili kuyatafuta yote yanayotendeka chini ya mbingu, na kuyavumbua kwa hekima; ni taabu kubwa ambayo Mungu amewapa wanadamu, ili kutaabika ndani yake.
14 Nimeziona kazi zote zifanywazo chini ya jua; na, tazama, mambo yote ni ubatili na kujilisha upepo.
15 Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa, Wala yasiyokuwapo hayahesabiki.
16 Nikatafakari nikisema, Nimejipatia hekima nyingi kupita wote walionitangulia katika Yerusalemu; naam, moyo wangu umeona kwa wingi hekima na maarifa.
17 Nikatia moyo wangu ili kuijua hekima, na kujua wazimu na upumbavu; nikatambua ya kwamba hayo yote nayo ni kujilisha upepo.
18 Yaani, Katika wingi wa hekima mna wingi wa huzuni,Naye aongezaye maarifa huongeza masikitiko.